Najaribu kutoroka nibatue haya makufuli, na kukata minyororo yenye kutu za muda ili nifunguke na shairi la ‘Vina Mpaka Uchina’. Laiti ningekuwa na fursa ya kupata wasaa toka kwenye kurasa hizi adhimu, ningeweza huandika hata kurasa mia mbili; kuzungumzia wimbo huu tu, ama mashairi ya hawa jamaa wa Miraba Minne.
Hili shairi lina aina ya mirindimo, sauti na fikra zinazonifanya niwaze. Kipindi kama hiki niwe na jamaa zangu wote, tumekaa pamoja maeneo fulani hususan Temeke, tunasikiliza huu wimbo kwa mshindo, sauti kubwa sana, labda kwa Juma Chaki (TMK Vetinari) pale au kona ya kwa Gogi.
Tunasikiliza tu, hatuongei wala nini, tunacheka tu na kugongeana, sababu maneno yanaingia moja kwa moja moyoni. Tunanesa na ute mzito wa besi, najifuta jasho la msimu wa kiangazi, tukibugia vumbi la mkito wa huu mdundo. Tunanesa na masingi ya snea za kutu, huku vibarua wa Kioo Limited wakigeuka mdogo mdogo kurejea makwao. Sahani (
hi hat) zikitatarika sawia na milio ya ndala za wapitao.
Mirindimo
Ushuhuda wa mirindimo ya besi unanisafirisha hadi utotoni nilivyotoroka kwenda kwenye ngoma ya Tokomile pale kwa Mama Zakia, Kigamboni Raha Leo. Kabla miembe iliyotukuka haijakumbwa na maangamizi ya njozi za maendeleo.
Tokomile ni ngoma ya wakubwa; huyu Teknohama aliyenyonga huu mdundo, ameamsha hizo hisia. Yaani besi inashabihiana na ngoma kuu inayoitwa Mlungula, unaopigwa na pandikizi la jitu (jitu la miraba minne). Hapo wababe wako na bakora zao na kila mtu ana puchali (jisu kubwa) kubwa kiunoni. Kwenye wimbo huu kimekosekana zumari tu, vinginevyo ingeleta madhari fulani matata sana. Unafahamu zumari ina mazingara mengi sana…
Nyanda za Ulimwengu
Maneno yanayosemwa kwenye ‘Vina Mpaka Uchina’ yananifanya nipate hisia ya kwamba, waliopo ulimwengu yabisi na wale waliopo ulimwengu ambao sio yabisi sote tujumuike ili tuburudike kwa pamoja. Wale waliopo ulimwengu si yabisi ni rahisi kufika hapa. Tayari tuko nao na hivyo kwao nasema ‘M.A.P. (Mungu Awaweke Pema)’. Ushanifahamu bwana?
Na wale walio katika ulimwengu yabisi, lakini bahati mbaya wako maeneo tofauti tofauti. Unajua upepo wa muda umetuzungusha na dhoruba zake, kila mtu yuko kona nyingine. Kuna walio Uchina, kama vile wimbo unavyoitwa ‘Vina Mpaka Uchina’, walio Bara la Ulaya, walio huko lizamako jua na kuandamia mwezi — sisi zamani tulikuwa tunawaita Wanyamwezi, siku hizi ni taifa jipya la Wajaluo kwa bwana Baraka Hussein wa Obama — wengine wako Australia na maeneo mbali mbali ya dunia. Wote tunajumuika kusikiliza hizi ngano za kitaa.
Vina Mpaka Uchina vinanipa mandhari ambayo ninaiona kabisa; nipo maeneo ya Salamanda (Mtaa Samora/Mkwepu, Dar) kabla jengo lililokuwepo pale halijakumbwa na dhoruba ya fitna za ukuwadi wa soko huria, kuna kijiwe tulikuwa tunakiita Ngazi Tano… Bado tumo kwenye maudhui ya Vina Mpaka Uchina na natumai tunakwenda sambamba.
Dimbwi la Kumbukumbu
Fitna za makuwadi wa soko huria zimesababisha majengo mengi kuvunjwa, hivyo mandhari ya mji mtukufu wa Mzizima (leo hii tunapaita Dar Es Salaam) imeanza kutoweka.
Huu wimbo unanirudisha siku fulani pale maeneo ya Salamanda, ndio kwanza narejea baada ya kusukumwa na upepo wa muda hadi linakozamia jua na kuangaza miali ya ajabu wakati wa kipupwe, huko Kaskazini ya Mwisho, Kanada. Nikagumiana na wana wawili wa kitambo sana,
Yusef Wamba na Hashim Dogo. Sasa, katika ujenzi wetu na shauku yangu ya kutaka kujua fani, Dogo akaniambia ‘hatufanyi tena sanaa’.
Mi’ nikahamaki hapo nikasema, ‘n’take radhi bwana, we una mamlaka gani ya kustahafu kabla yangu, hii kweli heshima?’ Huyu bwana anaitwa
Hashim Dogo na wakati wa ujenzi Yusef Wamba (wa Raiders Posse) alikuwepo pembeni yake. Hawa jamaa siwataji tu kiwepesi. Hawa ni watu mahiri sana kwenye huu ujenzi, na itasaidia wadau wengine wa fani kuona ninavyohusiana nayo.
Ikabidi niendelee kumuasa ya kwamba ni utovu wa heshima ya kitaa. Na kwa sababu yoyote inayonizuia mimi nisistahafu, basi yeye pia hana mamlaka ya kustahafu kabla ya mimi kufanya hivyo. Nikasisitiza kuwa hilo sio ombi bali ni amri.
Kwa vile heshima ya kitaa bado ipo, basi baada ya kutafakuri tukafikia muafaka. Kwa hiyo, tukatakana radhi na tukakubaliana kuendelea kujenga na kutumia njia mbadala za kuienzi hii fani. Kuwataja hao jamaa ni kuonesha kuwa lile jopo nitakalokuwa nimesimama nalo pale kwenye kona kwa Gogi, au kwa Juma Chaki TMK, au tuseme Salamanda Ngazi Tano (ambapo bahati imelinusuru jengo hilo), pembeni babu Kheri yupo na majarida bwena, m’ziki mnene… Hiyo ndio mandhari ninayopata ninaposikia mirindimo Vina Mpaka Uchina.
Twend’zetu
Sasa nirudi kwenye mada yetu, ngoja nikuongoze kwenye ulimwengu wa ngano za kitaa kupitia shairi la Vina Mpaka Uchina. Kwenye mstari wa kwanza Nash anaanza na kuingia na mantiki kwa mbali inayoshabihiana na athari za Shaaban Bin Robert. Nash amejitwika jukumu la ualimu, ilhali amekimbia darasa lake (la fani), hapa ameonesha anaweza kutengeneza hoja atapokabiliana na malenga.
Hii mantiki ya uandishi itagusa kwenye changamoto na mijadala mingi inayohusu ngano mbalimbali za ushairi. Sitaingia ndani sana kufikia labda mashairi ya Bi. Mwana Kupona (mshairi wa mahiri kale wa Pwani ya Mwambao wa Ukushi ya Mashariki, karne ya 17) au Fumo Liongo (mshairi mahiri wa kale Kanda ya Mwambao Ukushi ya Mashariki, karne ya 12), bali nitadodosa machache niyajuayo kadri ya uwezo wangu.
Kumekuwepo na mvutano baina ya ngano za mapokeo na ngano huria — sasa huu mfumo wa kupitia Hip Hop, mimi nauita ‘ngano za kitaa’. Kwenye miaka ya karibuni, enzi za Mohamed Ali Kibao, Mulokozi na Kezilahabi, kulikuwa na kambi mbili, ile ya mashairi ya mapokeo na mashairi huria. Mimi napenda kuwepo katikati ya hizi mantiki mbili. Navutiwa na mashairi ya mapokeo na bado safari yangu ya kujifunza bado ndefu sana. Wakati huo huo, upande huria naupokea ila kwa hadhari ya kanuni zitumikazo.
Sitokuwa na ule ‘ushabiki wa Kiulaya’ wa kuwa msanii anayechovya brashi kwenye rangi kadhaa na kuikung’utia kwenye ukuta, na baadae kazi kuuzwa kwa gharama za ajabu, la hasha. Hupenda kuwa na uzuri wa mambo ninayopenda, kuutambua kiuyabisi na kinadharia — yaani kifikra. Hivyo nakusihi uje nami msomaji. Hapa nasema twend’zetu, nataka nisikuache; uje usikie ule mpelampela wa mabomu ya Gongo la Mboto, mayowe ya wapiga debe na honi za daladala zinavyoweza kujibainisha kwenye mfinyango wa midundo ya kaka Teknohama, ambaye ni muandaaji wa mdundo wa wimbo huu, na ni mkazi wa Gongo la Mboto.
Kundi Hili
Miraba Minne ambayo ni mjumuiko wa wasanii binafsi wanne: Nash, PMC, Zaiid na Songa. Ni mkusanyiko wa vitongoji kadhaa vya jiji la Dar es Salaam. Nadhani juhudi hii waliyoifanya ni kuwahakikishia vichwa wa Hip Hop kuwa, ule uvumi uliokuwa ukienezwa kwamba Hip Hop ilihama Dar nyakati fulani ni porojo tu. Na ushahidi unajidhihirisha humu kwenye Vina Mpaka Uchina.
Na kwamba, hao washabiki walifunikwa tu na wingu la hadaa na upepo wa vina vya kitaa vilivyosukumwa sitiari za mbinde za msako wa ugali wa kutwa — vina vya mazingira hatarishi vimeweza kusukuma hilo wingu na hata mvua ikashindwa kunyesha. Huu muundo wa uandishi si mpya. Ni athari bayana za kizazi cha awali kwenye fani ya Hip Hop Tanzania, hususan Kwanza Unit. Hawa jamaa wanaandika kama wanachora na taswira inakuja na muundo wa nyanda tatu, ama ‘3D’ kwa lugha ya kigeni.
Nash
Ukavu wa sauti ya Nash nauhusisha moja kwa moja na lile vumbi la mtaa wa Mkamba, jirani na magereji ya Temeke Hospitali na maeneo yote yanayozunguka TMK, vumbi la sumu la viwandani kama Kioo Limited., Mabati na kadhalika. Ingawa Nash si muumini wa kudumu, athari za mila za Kiislamu zinasikika bayana, “Hii kasida si ya kuimba, tunaghani kiama”. Pia jina la wimbo (Vina Mpaka Uchina) yawezekana kuwa ni kumbukumbu za hadithi za masahaba wa Mtume, kama Ibuni Maja aliposema kuwa Mtume aliwataka masahaba zake na waumini wakaifuate elimu hata Uchina.
Nash anadhihirisha umahiri hapa: “Safina linakuacha, Maalim chata, haswa kwa darasa la Hip Hop; na hata madrasa alifu be, aisee shika ujiti nikubariki kinasa”. Hapa namuona kabisa Samia X na KBC wanachekea hadi wanashika mbavu na kusogeza wimbo nyuma. Maana sisi (jamii ya Kwanza) tunaita hii ‘kutoroka’; hapo alipomaliza ‘alifu be’ kawaida wengi wangetarajia amalize na ‘te’, jamaa akahama kabisa, akasema, ‘aisee shika ujiti!’ Ushaona eeh?
Songa
Bado kidogo Songa anichanganye maana kwenye mizunguko yangu ya awali sikumsikiliza kwa makini. Nilikuwa namvuka na kusikiliza majina niliyoyazoea. Sasa nikatega sikio mara moja, mwanzo ule mstari anavyoanza nilidhani anasema, “Vina mti ulio bora…” Akanihamisha, nikaona kama ameanza na kisa cha Adam na Hawa.
Baadae nikahakiki na kuelewa kuwa ni: “Vina, mke uliye bora”. Amegeuza vina kuwa mkewe na anamuusia. Hapo mwenyewe nilizimika. Hizi tafsida si mambo yanayokuja kiwepesi kama watu wanaoandika vimistari uchwara. Jamaa wanachimbuka mno kuweza kutengeza mistari mepesi madhubuti.
Songa ametokea kitongoji cha Tegeta, kwa wafahamu wa mambo, si habari mpya kuona isimu ya ushairi na mwambao wa Bahari. Sitaki kuongelea nadharia ya kuwa bahari yenyewe ndio inayosababaisha kuwepo ushairi mwambao, ila najua fika kuwa mazingira ya ushairi na mwambao ni jambo lenye isimu moja.
Sasa Songa kutoka Tegeta, ukijumlisha kuwa ni mwambao wa bahari, na yale mazingira yaliyopo kule lazima yanatengeza aina fulani ya fikra. Songa kama kabila nampa Uzaramo, maana ndio hugumzwa kuwa wana maneno mengi. Kwa mara ya kwanza kwenye historia ya ushairi Songa anadiriki kuisemesha taksi bubu: “Huu ni m’da wa kutubu, hadi taksi bubu leo itasema; nahusudu wema wa Mungu, naabudu kwa nguvu njema.” Kuna vile vina vya mumo kwa mumo ambavyo huleta ladha sana kwenye michano.
ZaiiD
Zaiid ni mzawa wa Mwenge, amezaliwa na kukulia Mwenge. Alipokulia ni mwendo wa dakika tatu wa mtu mzima toka ukumbi maarufu sana wa Mpakani Baa. Hapa ndio makao makuu ya ‘Kamanyola Bila Jasho wana wa Makwizi (Marqueez) du Zaire’. Yeye bila kujua huenda amepandikizwa huu uwezo wa michano ya kimirindimo.
Miezi 9 yake yote kabla ya kuzaliwa, miziki ilikuwa ikilia pale kwa sauti ya juu sana. Mitambao yake si namna zilizozoeleka kwenye redio kwa zama hizi za utandawizi, na ndio maana watu hata wasioongea Kiswahili bado huvutiwa na kumtafuta na kufanya naye mahojiano.
Fader ni gazeti mashuhuri sana Marekani, hata mimi nilishtuka nilipopigiwa simu na waandishi wa huko baada ya Zaiid mwenyewe kukosekana hewani kwenye namba yake ya Tigo.
Ule utundu wa kujitafsidisha na ngono ni namna ambayo bado itawasumbua sana wabadilishaji CD na watangavyaji (watangazaji wazinguaji) wa zama hizi, maana thamani ya ushairi ni jambo ambalo linatakiwa liwe kwenye damu ili kupata ladha zake kwa ufasaha.
Wengi wanaweza wakanasa kwenye mtego wa kishairi pale Zaiid anaposema, “Chana Kiingereza, mbongo utaishinda London? Nawapa kav’ kav’ ka’ tendo bila kondom.” Zaiid anaweza akakufanya udhani anaongelea ngono tokea alivyoanza, kwa kuwa amekaa kwenye maudhui hayo hayo. Nilichogundua ni kuwa Zaiid anaonesha jinsi alivyopania kujitoa muhanga; ngono bila kinga inasadikiwa ni kama kujiingiza kwenye balaa linaloweza kukufupishia maisha. Wakati huo huo anaasa, upande mmoja ubaya wa tendo hilo, huku akionesha alivyojitosa kuilinda na kuienzi fani ya Hip Hop na ushairi wa Kiswahili.
Namna alivyoshabihisha neno ‘London’ na ‘kondom’, ni somo linaloweza kusaidia wasioelewa vina. Kwenye hali ya kawaida hayo maneno huwezi kuyatumia hivyo, ila kwa mbinu ya matamshi iliyoshamiri, yeye ameifanya imekaa mule mule. Vina ni namna maneno yanavyotamkwa na mshabihiano wa kusikika na sio herufi tu kama wasanii wengi wanavyodhani. Zamani kwenye Hip Hop Marekani kulikuwa na msemo maarufu “You know the flava?”; anayeambiwa ama kuulizwa anaelewa ladha?
P The MC
Ninasikia bayana uimara wa vyuma vya reli aingiapo PMC, ukiona mchanaji anakwambia jambo ujue kuna namna anashabihisha, “Zima taarab weka Hip Hop; emcee mwenye ghadhabu nishafika, mchezo tafu basi chap chap kata nyika; ila ukicheza rafu nakupiga stop kama FIFA.”
PMC anawakilisha Kiwalani, na sistaajabu anapojiita bohari ya vina: “Unapigwa kwa mistari mi’ nd’o bohari ya vina; na nikishakuacha chali mentali habari sina”. Kiwalani imezungukwa na reli ya Tazara upande wote wa kaskazini hadi mashariki, upande wa magharibi ni eneo la uwanja wa ndege. Kiwalani ni moja ya maeneo ya watu waishio maisha ya mchaka mchaka. Maeneo ya namna hii huwa na athari ya moja kwa moja kwa jamii. Mara nyingi haya hujitokeza kwenye sanaa za ubunifu.
PMC toka nilipomsikia na kukutana nae kwenye WAPI hakuwahi kuniangusha, ni moja ya wasanii nilioona wazi kuwa ni hazina ya Hip Hop.
Hatimaye
Kiukweli siwezi kumaliza uchambuzi wa huu wimbo kwa makala moja. Nikipata fursa nitajaribu kuchambua beti hadi beti. Pia, kwa utashi wako msomaji, nia ya makala kama hizi ni kuonesha ama kuibua lulu ya fani iliyopo chini kabisa ya vina virefu. Kwa vile pumzi ninayo na maji nimeshayavulia, acha kwa leo niogelee humu humu tu na nikirejea nitakuwa nimeshaibuka toka mbizi au chomo (neno jipya nimejifunza toka kwa Songa) ya kuibua hizo lulu.
Kwa hiyo, kwa urefu wa kina hicho sitozama zaidi ya hapa. Nakaribisha maoni, nasaha na changamoto zote.
Nilidadisi watu wachache kupata maono yao ili isiwe ni mimi tu naikandamizia hii nyimbo kupita kiasi..
Mshafti
Nimezungumza na watu kadhaa kupata rai zao. Dada Sheila Ndila wa
Audio Kusini kule Kenya anasema hivi: “They did justice to the beat, they killed it already…hai-need refix, ishamalizwa.”
Kuna shabiki mwingine wa muziki anayeishi ughaibuni, Joyce Mategero, na maoni yake yalikuwa kama ifuatavyo: “Ushairi mkali sana, una kina haswa — na kweli Vina Mpaka Uchina. Ah nimewapenda sana. Heshima zao wabongo wanaondoka hatari.”
Wote hao wametoa miwa (kinasa sauti au maiki) mitano mitano kwa wimbo huu. Maoni ya hao ndugu hapo juu yalinisaidia kujihakikishia kuwa sikuwa nashobokea tu hawa madogo — ni kuwa Vina Mpaka Uchina ni aina ya wimbo unaoweza kukusafirisha masafa ya mbali sana. Kwa heshima na taadhima nagotea hapo.
Pamoja!