Chimbuko la Hip hop linaweza kufafanuliwa kwa kifupi kama ‘juhudi za wasiojiweza’. Hili lilionekana dhahiri wakati Wamarekani weusi walipokuwa wakipigania haki zao za kijamii, wakati huo wa civil rights movement. Hapa kwa haraka tunaona uhusiano wa Hip Hop na jamii. Hip Hop ikiwa upande wa wanyonge, ikitumika kama sauti ya wakandamizwaji.

Miaka hiyo imekwishapita na muziki huu umekua na kuwa ni utamaduni. Lakini bado umebaki na damu ya uanaharakati. Hip Hop imebadilika kama tamaduni yeyote ile, na mpaka kuvuka mipaka. Mipaka hiyo ilivuka hadi kufika Tanzania ambako ilikaribishwa. Boardman anajenga hoja kuwa, Hip Hop ilifanikiwa kuvuka mipaka ya Tanzania kutokana na kuanguka kwa Siasa ya Ujamaa. Mwanzo ulikuwa mgumu, na bado safari ni ndefu, lakini mafanikio yanaonekana; kama kukubalika na jamii.
Muziki huu hata hivyo bado unaonekana kama ni tamaduni ya Kimarekani zaidi, huku kuna baadhi ya watu kwenye jamii zetu ambao wanaona Hip Hop ya nyumbani ‘ina-recycle’ tu yale yanayofanywa na wasanii wa Marekani. Kwenye hilo natumaini kuwa kila mtu atakuwa na mawazo yake, lakini ili kupata jibu lililo karibu na sahihi, ni vizuri kurudi kwenye chimbuko la tamaduni wa muziki huu wa Hip Hop.
Muziki huu ulikuwa unaitwa “muziki wa kufokafoka” kipindi hicho. Nadhani hilo jina halikuwa sahihi, na uliupa mziki huu taswira mbaya. Lakini kwa kuwa ulikuwa ni muziki mpya, inawezekana hatukujua jina gani litakuwa sahihi. Hata hivyo, ukiangalia kwa karibu labda neno kufoka halikukosea sana, kwani kurap ni kama kufoka — lakini neno sahihi la Kiswahili ni kughani.
Muziki huu ulileta mgongano kati ya kizazi chetu na kizazi cha Tabora Jazz kwani muziki huu uliangaliwa kwa tafsiri tofauti. Muziki huu ulionekana ukiwa na hiyo dhana ya kufokafoka, na kawaida ya tamaduni zetu, mtoto hamfokei mzazi. Hivyo inawezekana Hip Hop ikaonekana ni muziki unaochochea uasi dhihi ya tamaduni zetu za ndio mzee. Lakini kwa upande mwingine, hasa ukiangalia katika chimbuko, huu ni muziki wa watu wanaokandamizwa. Hivyo kipindi kile cha akina II Proud na Wapi Tunakwenda, vijana tulikuwa na madukuduku mengi.

Hip Hop ikafanya vile vile kama ilichofanya Marekani kipindi cha miaka ya sitini na sabini — kuwapa wanyonge sauti. Tofauti ilikuwa, huko Marekani iliwapa watu weusi (hasa vijana) sauti dhidi ya ubaguzi wa rangi. Hapa Tanzania, suala halikuwa ubaguzi wa rangi, lakini kupigania haki za vijana, dhidi ya uonevu wa polisi, dhidi ya maisha magumu kwa vijana n.k. Hivyo ni kweli, mwanzoni kwenye hip hop watu walikuwa wanafoka vilivyo, kwani matatizo yalikuwa mengi na hakuna aliyewasilisha matatizo hayo ya vijana, au hata kuyapa nafasi ya kusikilizwa. Hilo linafanana na makundi kamaN.W.A. huko Marekani. N.W.A walikuwa wakali, kwani hali halisi yao ilikuwa ni ngumu sana kipindi hicho, ukilinganisha na sasa.
Sasa kama tamaduni nyingine, Hip Hop imekuwa inakwenda na wakati, pamoja na kuwa kwenda na wakati huko hakujasaidia sanaa hii moja kwa moja. Maisha yamebadilika, vijana wa juzi waliokuwa wanapigania haki zao, leo baadhi wamefanikiwa. Hivyo maudhui ya mashairi yamebadilika kwa namna moja au nyingine. Kama marekani, vijana wengi wametajirika kupitia mgongoc wa Hip Hop, hivyo kuanza kughani kuhusu utajiri wao, kwasababu hawaishi tena kwenyeghettos kama awali.
Hapa Tanzania, kwenye nchi masikini, Hip Hop imekuwa bado ikitegemewa katika kutetea haki za wanyonge na kuzungumzia matatizo ambayo yanaendelea kukabili vijana wengi. Pamoja wapo wachache, waliofanikiwa, wengi wa vijana bado wapo kwenye hali ngumu. Hapa ndipo neno “Hali Halisi” linapoingia katika kuchambua Hip Hop ya Tanzania. Wapo ambao wanahesabiwa kama si wana Hip Hop, kwani mashairi yao hayazungumzii hali halisi ya maisha ya kijana wa kila siku wa Kitanzania. Hili linaendana na picha zilizomo kwenye video nyimbo zao. Video nyingi zinaonekana kushindwa kuakisi yaliyomo katika tamaduni zetu, bali huakisi zaidi yaliyomo katika mila na desturi za tamaduni za Magharibi.
Hili suala la mila na desturi ni mjadala mwingine, kwani video hizi huonekana kama zinakiuka maadili ya mila na desturi zetu. Mengi yamezungumzwa, bila kufafanua nini maana ya mila na desturi zetu, kwani kama suala ni mavazi ya uchi,basi kuna Wamasai ambao hutembea wamevaa lubega tu, bila kuwa na mavazi ya ndani. Wapo wengine ambao wanaona picha za kwenye video za Hip Hop zinahamasisha maovu; kwa mfano ngono, kama vile video nyingi za Hip Hop za Marekani. Kama hilo ni tatizo, basi tunaweza kubadilishakituo cha runinga na kuweka mduara, ambao naamini ni tamaduni yetu.