facebook

Monday, January 4, 2016

SOMA HAPA WALAKA WA MALLE HANZi KWA KALA PINA.

NI  MAPEMA  SANA KALA PINA!!!!

Kalama  Masoud  Suleiman  ndio  jina  halisi  la  mtu  ambaye  anafahamika  kama    Kala  Pina,  Nabii Koko,  Kamanda  Mura,  Mbunge  Mtarajiwa  n.k.  Licha  ya  Kalama  Masoud  kuwa  na  ‘a.k.a’  nyingi  ni ‘a.k.a’  moja  tu  ambalo  inatambulika  zaidi  ambayo  ni  Kala  Pina.  Kwa  mujibu  wa  maelezo  yake mwenyewe  anasema  “maana  ya  Pina  ni  kitu  kipya..  kwa  hiyo  Pina  anakuwa  mpya  kila  siku, hawezi  kuwa  yule  yule  wa  zamani”  (clouds,  2015).

Kabla  ya  kuzama  katika  ulingo  wa  siasa  za  vyama,  Kala  Pina  amekuwa  katika  sanaa  ya  muziki akijikita  katika  mapambano  ya kuisimamisha  Hip  Hop  nchini  Tanzania.  Hakuna  rekodi  za  uhakika ambazo  zinaonesha  ni  lini  hasa  Kala  Pina  alianza  kufanya  muziki  ila  kuna  uwezekano  akawa ameanza baada  ule  wakati  ambao  Chid  Benz  aliousema  kwamba    “alianza  muziki  Hashim  bado anachana…  Profesa  mwembamba…  Kala  Pina  anauza  flana”  katika  wimbo  ambao ameshirikishwa  na  Ay  na  Mwana  FA.

Kauli  hiyo  inaweza  kuwa  sababu  iliyochochea  pia  kutokuelewana  kwa  Kala  Pina  na  Chid  Benz kiasi  cha  Chid  Benz  kupokea  ‘nakozi’  miaka  ya  hivi  karibuni  kutoka  kwa  pina.  Kwa  ujumla  Kala Pina  ni  msanii  ambaye  sanaa  yake  zinapambwa  na  ubabe/nguvu  kama  mbinu  ya  ukombozi ambao  unasadifu  kabisa  jina  la  kundi  lake,  Kikosi  Cha  Mizinga  chenye  maskani  yake  Kinondoni Block  41.  Kwa  hivyo  kutofautiana  na  Kala  Pina  muda  mwingine  ni  kama  “Kujitoa  mhanga  zaidi ya  yesu  msalabani”  kama  yeye  mwenyewe  alivyosema  kwenye  ‘Umoja  ni  Nguvu’  huwezi kitakupata  nini  ukithubutu  kukutwa.

Katikati  mwa  Miaka  ya  2000  kuelekea  mwishoni  ambapo  marapa  wengi  walipoanza  kufanya nyimbo  za  siasa  zikiitaja  moja  kwa  moja  serikali  ama  majina  ya  viongozi  wake.  Kwa  wengi kilionekana  ni  kitu  kipya  lakini  Kala  Pina  aliwahi  kukaririwa  akisema  katika  mahojiano  na  kituo kimoja  cha  redio  akisema  kwamba  yeye  alichana  waziwazi  viongozi  wa  serikali  miaka  mingi iliyopita  katika  kibao  cha  ‘Tunasonga’  aliposema  kwamba  yuko  “Tayari  kukipaka  hata  mbele  ya bwana  mkapa”.

Kala  Pina  sio  rapa  wa  kwanza  ambaye  aliweza  kuwachana  viongozi  moja  kwa  moja  katika nyimbo  ikumbukwe  katika  makala  moja  hivi,  zavara  (2012)  aliwahi  kusema  kuwa  mwishoni  mwa miaka  ya  80  (kama  sio  88)  msanii  aitwaye  Dika  Shap  aliwahi  kufanya  wimbo  ambao  alimuimba Raisi    wa  wakati  huo  Ndugu  Ali  Hassani  Mwinyi.  Tofauti  ya  miaka  inamfanya  Dika  Shap  awe mchanaji  wa  mwanzo  mwanzo  kumchana  kiongozi  wa  juu  wa  serikali.

Baada  ya  kuchana  katika  muziki  mambo  ya  siasa,    katika  uchaguzi  wa  Mwaka  2010  Kala  Pina aliamua  kujitosa  katika  majukwaa  siasa  kugombea  udiwani  kupitia  chama  cha  wananchi  CUF.   Katika  uchaguzi  huo  Pina  alishindwa  kwa  sababu  anayoieleza  kwamba  “lililopofika  zoezi  la   kuhesabu  kura  ghafla  aliingiwa  na  kitu  jichoni  na  kupata  maumivu  makali  mno  na  kukimbilia nyumbani  watu  walipomuangalia  hawakuona  kitu  na  baada  ya  kufanya  dua  alipata  nafuu  na kurudi  kituo  cha  kupigia  kura,  akakukuta  mambo  yameshaharibika”  (Ayo,  2015).

Pina  anasema  jicho  hilo  lilimuuma  kwa  sababu  za  kishirikina  (yeye  akiziita  sababu  za  kimila  na kitamaduni).  Katika  mahojiano  aliwahi  kuulizwa  kama  ni  kweli  siasa  inahusishwa  sana  na  imani za  kishirikina  akajibu  “hayo  ni  mambo  ya  mila  na  utamaduni  yapo  dunia  nzima..  tena  kwenye siasa  yana  nafasi  kubwa  sana  kwa  sababu  ni  masuala  ya  utawala”.  Alipoulizwa  kwamba  kama yeye  (Pina)  anaye  mganga  wake  alikwepa  kujibu  swali  hilo  lakini  katika  uchaguzi  wa  2015 alisema  atajipanga  kwa  mitindo  yote  ya  kisayansi,  kiutamaduni,  kiuchumi  n.k  kutokana  na kuingia  kichwa  kichwa  kwenye  uchaguzi  wa  2010  (Clouds,  2015).

Baada  ya  kushindwa  mara  ya  kwanza,  Kala  Pina  alisema  kwamba  atajipanga  kiutamaduni, kiuchumi,  kisayansi  n.k  lakini  nafikiri  hakujipanga  kikamilifu  kutokana  na  kushindwa  tena  katika uchaguzi  wa  2015  na  safari  hii  akigombea  ubunge  wa  Kinondoni.  Safari  hii  pia  aligombea  kupitia chama  kipya  cha  ACT.  Sababu  ya  kuhama  CUF  kwenda  ACT  wakati  alishiriki  michakato  yote kutafuta    mgombea  atakayesimamishwa  kugombea  ubunge  jimbo  la  Kinondoni  hazifahamiki. Sijui  ni  nini  kilitokea,  labda  jina  lake  ‘lilikatwa’  katika  mchakato  wa  kutafuta  mgombea  akaona atimkie  ACT  au  hakupenda  Lowassa  kujiunga  na  UKAWA  akaamua  kung’atuka.

Ikumbukwe  niliwahi  kuandika  kwamba  “Kala  Pina  alishindwa  kupiga  hesabu  zake  vizuri  kwa sababu  chama  alichokihama  (CUF)  na  kwenda  ACT  ndicho  kilichoshinda  uchaguzi.  Kwa  lugha  ya mtaani  tunasema  alichengana  au  alipishana  na  gari  la  mshahara”  (Hanzi,  2015).  Nilimtazama katika  Luninga  baada  ya  matokeo  kutangazwa  alihojiwa  akasema  anapinga  matokeo  hayo  na amekataa  kusaini  kutokana  uwepo  wa  mapungufu  hususani  zoezi  la  kuhesabu  kura.

Licha  ya  Mapungufu  katika  mchakato  wa  uchaguzi  aliyoyaeleza  nafikiri  sababu  ya  kushindwa ambayo  ingemfaa  zaidi  Kala  Pina  ni  ile  aliyosema  Afande  Sele  kwamba  “watu  wengi  hawakuwa wanakifahamu  chama  alichokuwa  akigombea”  (Ayo,  2015)  ambacho  ni  ACT  alichomo  Kala  Pina kutokana  na  uchanga  wake  katika  medani  ya  siasa.  Pia  niliwahi  kusikitika  jinsi  ulivyojibu  swali uliloulizwa  kwamba  ungekuwa  ndani  ya  bunge  wakati  wa  sakata  la  escrow  ungefanyaje  ukajibu kwamba  ungetoa  kichapo  bungeni  kwa  sababu  ya  kinga  ya  wabunge.  Nadhani  pia  wananchi waliangalia  pia  uwezo  wa  kujenga  hoja  na  kupangua  hoja.

Baada  ya  uchaguzi  wa  udiwani,  ubunge  na  uraisi  kuisha  na  Dkt  John  Pombe  Maghufuli kutangazwa  na  kuapishwa  kuwa  Raisi  wa  Tanzania  Kala  Pina  ameibuka  na  kitu  kipya  tena  kama ambavyo  jina  lake  lilivyo.  Hivi  karibuni  ametoa  wimbo  ambao  umelenga  kusifia  utendaji  kazi  wa raisi  Dkt  Magufuli  ambaye  toka  aapishwe  hajatimiza  hata  miezi  mitatu.  Nakiri  kwamba  ni  kitu kizuri  ambacho  kinaweza  kumtia  morali  ya  kazi  mheshimiwa  kuendelea  kuwatumikia watanzania  kwa  “kiwango  cha  lami”  lakini  waswahili  hawakukosea  pia  kusema  “Mgema akisifiwa,  Tembo  hulitia  maji”.

Kwenye  huu  wimbo  Kala  Pina  licha  ya  kumsifia  sana  Dkt  Magufuli  lakini  kuna  sehemu  anasema anaona  kama  Miujiza  kwa  vitu  vinavyoendelea.  Hatua  ambazo  anazozichukua  magufuli  ni  nzuri japo  ni  robo  ya  robo  ya  robo  ya  hatua  ambazo  zinapaswa  kuchukuliwa.  Miujiza  ni  magufuli kutenda  kile  ambacho  wapinzani  walitaka  kufanya.  Ila  miujiza  mingine  ni  pale  Kala  Pina  ambaye ni  mpinzani  wa  chama  tawala  anaposema  “wapinzani  wamefungwa  kufuli  wamekosa  cha kusema”.  Najiuliza  tu  Kala  Pina  yuko  chama  cha  upinzani  au  yuko  chama  tawala.  Kama  yuko Upinzani  kwanini  asiseme  “wapinzani  tumefungwa  kufuli”  na  yeye  akajijumuisha.

Kala  pina  anasema    miaka  yote  ambayo  amefanya  muziki  hajawahi  “kumsifia  mtawala  lakini kwa  magufuli  hilo  halina  mjadala”  uzalendo  umemshinda.  Kala  Pina  anamchukulia  maghufuli kama  mzalendo  ambaye  hajatokea  miaka  mingi  na  amekuja  kama  mkombozi  tuliyemngoja miaka  kadhaa.  Ni  jambo  zuri  kusifia  lakini  nimkumbushe  Kala  Pina  mambo  yafuatayo:-

Mtatiro  (2015)  alishawahi  kusema  wanaomkosoa  magufuli  hawana  cha  kupoteza  ili  mradi wanasema  ukweli  na  unapaswa  kufanyiwa  kazi.  Hawa  ni  watu  wanaoiona  dunia  ya  mbele  na kuiishi  sasa  na  wanaomtetea  magufuli  kwa  kila  kitu  hawa  watajifunza  pindi  watakapoifikia dunia  ya  mbele.  Akaendelea  kusema  “anachofanya  magufuli  leo  kiliongelewa  jana    na  juzi  na wakosoaji,  waliishi  jana  na  juzi  lakini  waliiona  dunia  ya leo”.

Kaka  Kala  Pina  asije  kuwadharau  wakosoaji  wa  magufuli  kwa  sababu  “ndiyo  chanzo  cha mabadiliko  duniani,  hawa  ni  watu  wanaohoji  kila  kitu  mpaka  wanaingia  kaburini.  Hawa  ni  watu ambao  watapiga  kelele  kupinga  safari  za  nje,  ukizifuta  watapiga  kelele  kuhoji  pesa  za  safari zilizokatwa  zimekwenda  wapi,  hawa  ni  watu  watakaoenda  mbali  kutaka  kuwepo  na  sharia  za kuelekeza  safari  za  nje,    na  ukiwatungia  sharia  watakuja  mbele  kuhoji  kama  kweli  itajenga misingi  waliyoipigia  kelele,  ukishatunga  watakuja  kukosoa  inahitaji  marekebisho,  ukiifanyia marekebisho  watakuhoji  mbona    huitekelezi  ipasavyo,  na  ukianza  kuitekeleza  watakuuliza imeleta  manufaa  gani…”  (Ibid).

Nikukumbushe  pia  Nas  Escoba  alishawahi  kusema  “trust  no  black  leaders”  akiwa  na  maana usimwamini  kiongozi  mweusi.  Viongozi  weusi  wengi  wamekuwa  vibaraka  wa  nchi  za  magharibi. Usisahau  kwamba  Obama  ni  mtu  mweusi  lakini  yeye  na  wenzie  ndio  waliomuua  Ghadafi  huku viongozi  wote  wa  nchi  za  Kiafrika  hakuna  aliyetoa  msaada  wowote  hata  kwa    kukemea  tu uvamizi  huo.

Immortal  Technique  ni  mchanaji  ambaye  Kala  Pina  huwa  anajilinganisha  nae  kiitikadi  aliwahi kusema  “Capitalism  and  Democracy  are  not  synonymous”  kwamba  neno  “ubepari  na demokrasia  sio  maneno  mbadala”  ila  mabepari  huyalandanisha  ili  kusambaza  demokrasia  yao. Kimsingi  kila  nchi  inatakiwa  kuwa  na  demokrasia  yake  ikiwa  tu  wananchi  wenyewe  ndio wameamua  demokrasia  hiyo.  Sisi  Tanzania  tumeshapoteza  demokrasia  yetu  miaka  mingi, mambo yetu mengi  yanaamuliwa  nje.

Kimsingi  hizi  pongezi  kupitia  wimbo  huu  wa  Kala  Pina  zimetoka  mapema  sana  raisi  akiwa hajamaliza  hata  miezi  mitatu  ofisini.  Kilichofanyika  ni  kama  kumpa  msanii  tuzo  ya  wimbo  bora wakati  bado hajaurekodi. ungesubiri  2020  ndipo ungeweza  kufanya  tathmini  yakinifu  tofauti  na  hapo  wengine  wanaweza  kuona  kama  “sizoni  twu ya  kampeni”.  Mapema  yote  hii  amemsifia  vipi  huko  mbele  akabadilika  na  mambo  yakawa ndivyo  sivyo…  itakuaje? au utawaeleza nini tena watanzania.

Nimalize  kwa  kunukuu  maneno  haya  yanayosema  kwamba  “Kiongozi  mwerevu  hana  cha kujifunza  kwa  waridhikaji,  wapongezaji  na  wakubali  kila  kitu”  (Mtatiro,  2015).  Kwa  hivyo tuendelee  kukosoa  kwa  kadri  inavyowezekana  na  pia  tusifie  pale  inapobidi  lakini  kwa  umakini   na  tahadhari  ili  tusivuke  mipaka  ya  pongezi.  Pongezi  za  Kala  Pina  zimetoka  mapema  sana… angesubiri  subiri  kidogo.  Dkt  Magufuli  ana  majipu  mengi  ya  kutumbua  na  nikikutajia  utaona kama bado  hajaanza kazi. Heri ya mwaka mpya. Cheers.

Imeandikwa  na
Malle  Hanzi
O715076444
©2016

No comments:

Post a Comment